Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Hawza, majlisi hizo zimeendelea kufanyika katika eneo la Kigogo Posti, jijini Dar es Salaam, ambapo wakinamama kutoka maeneo mbalimbali wamekusanyika kwa ajili ya kuhuisha kumbukumbu ya shahada ya Imam Hussein (as), mjukuu wa Mtume Muhammad (saww), aliyeuawa kwa dhuluma pamoja na masahaba na watu wa familia yake katika jangwa la Karbala.
Katika mazingira yaliyojaa simanzi, machozi na tafakuri juu ya msimamo wa Imam Hussein (as) dhidi ya dhuluma na uonevu, washiriki wa majlisi hizo wameendelea kupata mafunzo mbalimbali ya kidini, kijamii na kimaadili yanayolenga kuimarisha imani, malezi bora ya familia na kujenga kizazi kinachofuata njia ya haki na uadilifu.
Aidha, wahadhiri mbalimbali wa kike wamewasilisha darsa na mawaidha tofauti yanayohusiana na tukio la Karbala na shahada ya Imam Hussein (as), wakibainisha nafasi muhimu ya wanawake katika kulinda na kueneza ujumbe wa Ashura, hususan kupitia mifano ya kishujaa ya Bibi Zainab Kubra (as) na wanawake wengine wa Karbala.
Washiriki wa majlisi hizo wameeleza kuwa maombolezo ya Imam Hussein (as) si tukio la kihistoria pekee, bali ni shule ya kudumu inayofundisha kusimama upande wa haki, kupambana na dhuluma na kulinda maadili ya Kiislamu katika kila zama.
Majlisi za maombolezo ya Imam Hussein (as) zinaendelea kufanyika katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania sambamba na kuwadia kwa siku za Ashura, huku waumini wakizidi kuhuisha ujumbe wa Karbala kwa hamasa kubwa, mapenzi ya dhati kwa Ahlul-Bayt (as) na huzuni ya kuikumbuka shahada ya Sayyid al-Shuhadaa Imam Hussein (as).








Maoni yako